Hii hapa namna ya kujikinga na Mpox

Wizara ya Afya imewahimiza wananchi kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa wa Mpox kwa kuepuka kushiriki vitu vya binafsi kama nguo, mashuka na blanketi vilivyotumiwa na mtu mwenye dalili za ugonjwa huo.
Pia, wananchi wanashauriwa kuepuka kugusana, kushikana mikono, kubusiana, kukumbatiana au kujamiiana na mtu mwenye dalili za Mpox. Aidha, inasisitizwa kuepuka kugusa majimaji ya mwili ya mgonjwa au kumhudumia bila kuchukua tahadhari zinazostahili.
Wizara imewataka watumishi wa afya kuzingatia kanuni za kujikinga na magonjwa wanapowahudumia wagonjwa, hususan wale wenye dalili za vipele na homa.
Tahadhari nyingine ni kuhakikisha unawanawa mikono mara kwa mara kwa maji na sabuni au kutumia vitakasa mikono ili kujikinga na maambukizi.
Wagonjwa Wawili Wathibitishwa Kuwa na Mpox
Katika taarifa iliyotolewa leo Machi 9, 2025, na Waziri wa Afya, Jenister Mhagama, watu wawili wamethibitika kuwa na ugonjwa wa Mpox. Mmoja wa wagonjwa hao ni dereva wa magari ya mizigo aliyesafiri kutoka nchi jirani kuelekea Dar es Salaam.
Dalili za Mpox
Dalili za ugonjwa huu ni pamoja na:
- Vipele mwilini
- Homa
- Maumivu ya kichwa
- Vidonda kooni
- Maumivu ya viungo, misuli na mgongo
Wizara inawashauri wananchi wanaopata dalili hizi kufika katika kituo cha afya kwa uchunguzi na matibabu au kupiga namba 199 bila malipo kwa msaada zaidi.
Hakuna Mgonjwa Mpya wa Marburg
Kuhusu ugonjwa wa Marburg, Waziri Mhagama amethibitisha kuwa hadi Machi 1, 2025, hakuna mgonjwa mpya aliyeripotiwa.
CHANZO;O NIPASHE
Comments
Post a Comment